logo

NOW ON AIR

Listen in Live

RIP! Seneta Wa Baringo William Cheptumo Afariki

Cheptumo aliaga dunia akiwa katika Hospitali ya Nairobi, ambako alikuwa akipokea matibabu.

image
na Samuel Maina

Yanayojiri16 February 2025 - 14:01

Muhtasari


  • Kwa mujibu wa familia yake, marehemu alikuwa akiugua kwa muda mrefu hadi kufariki tarehe 16 Februari.
  • Rais Ruto ameomboleza kifo chake, akimtaja kama kiongozi mwenye maono na aliyejitolea kwa maslahi ya wananchi.

Marehemu Seneta Wa Baringo William Cheptumo

Seneta wa Kaunti ya Baringo, William Cheptumo, amefariki dunia.

Cheptumo aliaga dunia akiwa katika Hospitali ya Nairobi, ambako alikuwa akipokea matibabu kwa ugonjwa ambao haukuwa wazi kwa umma.

Kwa mujibu wa familia yake, marehemu alikuwa akiugua kwa muda mrefu hadi kufariki tarehe 16 Februari.

Mmoja wa famili yake alifichua kuwa wiki iliyopita aliruhusiwa kutoka hospitalini, lakini hali yake ilidhoofika tena, jambo lililomfanya arudishwe hospitalini.

Rais William Ruto aliongoza taifa katika kuomboleza kifo chake, akimtaja kama kiongozi mwenye maono na aliyejitolea kwa maslahi ya wananchi.

"Cheptumo alikuwa mzalendo, mchapakazi na mtetezi wa maendeleo ya Baringo. Tunawapa pole familia yake, marafiki na wakaazi wa Kaunti ya Baringo," Rais aliandika kupitia mtandao wa X.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hifadhi ya wafu ya Lee Funeral Home.

Marehemu Cheptumo, aliyekuwa na umri wa miaka 57, alikuwa wakili kwa taaluma na alihudumu kama Mbunge wa Baringo Kaskazini kati ya mwaka 2008 na 2013.

Katika Uchaguzi Mkuu wa 2022, alichaguliwa kuwa Seneta wa Baringo kupitia chama cha UDA, akimshinda Gideon Moi wa KANU.

Alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama wa Kitaifa, Ulinzi na Masuala ya Kigeni katika Seneti.

Cheptumo pia alikuwa mwanzilishi wa kampuni ya uwakili ya Cheptumo and Company Advocates.

Kabla ya kujitosa kwenye siasa, alifanya kazi kama afisa wa sheria katika Benki Kuu ya Kenya na Shirika la Maendeleo ya Viwanda na Biashara (ICDC).

 Alipata shahada ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, kisha akasomea diploma ya uzamili katika sheria katika Chuo cha Sheria cha Kenya.

 Safari yake ya elimu ilianza katika Shule ya Msingi ya Maregut (1975-1981), ambako alipata Cheti cha Elimu ya Msingi (CPE).

 Baadaye, alijiunga na Shule ya Upili ya Bartolimo (1982-1985) kwa masomo ya sekondari ya chini, kabla ya kuendelea na elimu ya sekondari ya juu katika Shule ya Upili ya Kabarnet mnamo 1986.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved