Naibu mwenyekiti wa Jubilee David Murathe amesema ana imani kuwa Raila Odinga atapokea kura nyingi kutoka Mt Kenya kuliko zile za ngome yake ya kisiasa.
Murathe alisema amepima hewa na kuona kuwa wakazi wa Mt Kenya watamkumbatia Raila kuliko hata eneo la Nyanza.
Akiongea na runinga ya KTN, Murathe alisema watahakikisha kuwa Raila ndiye atapokea kura za kutosha ili kumshinda hasimu wake William Ruto.
Aidha aliongeza kuwa si lazima Raila apokee kura za Mt Kenya ili kushinda urais akisema bado kikapu chake cha 2017 kimejaa.
"Watu hawa (timu ya Kenya Kwanza Alliance) wamedhania mchezo wao wote kuhusu kura za Mlima Kenya lakini hata bila kura za Mlima Kenya, Raila bado atakuwa Rais," alisema Murathe.
Alisema kuwa Naibu Rais William Ruto angali afisini leo kwa sababu analindwa na Katiba.
Mapema mwaka huu, Murathe alidai kuwa Rais Uhuru Kenyatta alikatisha mazungumzo yake na William Ruto kwa sababu Naibu Rais alikuwa na nia ya kuhujumu utawala wake.
Akizungumza mjini Thika, Murathe alisema kuwa Ruto alipewa nusu ya serikali zikiwemo baadhi ya wizara zenye nguvu lakini Rais hakuridhishwa na jinsi zinavyoendeshwa.
Mbunge huyo wa zamani alisema Uhuru aliamua kufanya kazi na Raila ili kuhakikisha kile alichotaka kuwafikishia Wakenya kinatimizwa.
Rais Uhuru anamuunga mkono Raila huku akitaka eneo la Mt Kenya kumpigia kura ifikapo mwezi Agosti ili kuchukua mamlaka.