Mbunge wa muda mrefu wa Garissa Mjini Aden Duale ametangazwa kuwa mshindi waceneo bunge hilo kwa mara ya nne mfululizo kupitia chama cha UDA huku akimbwaga mshindani wake wa karibu Nasir Dolal aliyekuwa anamtoa kijasho kupitia chama cha ODM.
Mbunge huyo, mfuasi shupavu wa DP William Ruto na aliyekuwa kiongozi wa wengi alipata kura 9,905 dhidi ya kura 5,972 za Nasir.
Mapema mwaka jana Duale baada ya kung’atuliwa katika wadhfa wake wa kuwa kiongozi wa wengi kwenye bunge la kitaifa kwa kuegemea mrengo wa naibu rais William Ruto alitangqaza kwamba hangewania tena ubunge bali jukumu lake kuu lilikuwa ni kuhakikisha anampigia debe naibu rais Ruto ili atakaposhinda yeye atapata nafasi ya kujivinjari kwenye ikulu kifahari akinywa chai.
Duale aling’atuliwa katika mageuzi ambayo yalionekana kuwa ni mabadiliko rais Kenyatta alikuwa anafanya kwa kuwaangushia shoka la ghadhabu wabunge na viongozi waliokuwa wanaegemea mrengo wa naibu rais jambo lililotishia kusambaratika kwa chama cha Jubilee.
Nafasi yake ilikabidhiwa mbunge anayeondoka wa Kipipiri Amos Kimunya ambaye pia jana ametangaza kukubali kushindwa katika jaribio lake la kutaka kuwa mbunge wa eneo hilo kwa mara ya nne mfululizo pia kama Duale.
Wengine ambao Duale alikuwa anamenyana nao katika kinyang’anyiro hicho ni pamoja na Abdullahi Mohamed wa UPIA aliyepata 5,529 na kumaliza nambari tatu na Siyad Osman alipata kura 952 akifunga nne bora.