Kocha mkuu wa KCB Patrick Odhiambo amewasifu wachezaji wake baada ya kulaza Talanta 2-1 katika uga wa Dandora jijini Nairobi mnamo Ijumaa.
Ushindi huo uliwapelekea kufikisha alama 20, na kuwasaidia kujikita kileleni mwa Ligi Kuu ya Kenya.
"Tulicheza vyema sana na tulistahili ushindi. Nina furaha tulifanikiwa kurejea kwa nguvu kutoka kwa kushindwa kwetu na Mathare United wiki jana. Vijana wanastahili kutambuliwa kwa juhudi zao," alisema.
"Kama timu nyingine yoyote kwenye mashindano tunatamani kunyanyua kombe mwishoni mwa msimu lakini hatuwezi kujiruhusu kutawaliwa na shinikizo la kutwaa ubingwa. Tunaangazia mechi moja kwa wakati, " Odhiambo alisema.
Huku Odhiambo akishangilia ushindi huo, kocha mkuu wa Talanta Jackline Juma alihusisha kushindwa kwao na ukame wa mabao.
"Tulifanya kila tuwezalo katika mechi hiyo lakini ninaamini tulipaswa kufanya vyema zaidi. Wakati ujao tutahitaji kuacha kupoteza nafasi za wazi ikiwa tunataka kushinda mechi," alisema.
Francis Kahiro aliifungia KCB bao la kuongoza dakika ya 18 baada ya kuandaliwa Paso murwa na kiungo mkabaji James Kinyanjui.
Bao hilo lilikuwa lake la sita msimu huu. Wanabenki hao walihitaji tu bao la kichwa kutoka kwa Maurice Ojwang katika dakika za lala salama ili kupata ushindi huo muhimu.
