Hatimaye baada ya ngoja ngoja za kutambua wanariadha bora wa mwaka 2024 duniani kote, Letsile Tebogo na Sifan Hassan ndio wameshinda tuzo hizo upande wa wanaume na wanawake mtawalia.
Washindi hao ambao ni mabingwa kwenye mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika nchini Ufaransa, walishinda tuzo hizo katika gafla iliyofanyika Monaco kwa kupigiwa kura na mashabiki wa riadha kote duniani.
Tuzo za shirikisho la riadha duniani za kila mwaka hufanywa ili kuwatambua wanariadha wanaofanya vyema katika mashindano mbali mbali ikiwemo mashindano ya Olimpiki ambapo tuzo hizo hugawanywa kwa vitengo vitatu.
Katika tuzo zilizotolewa Jumapili jioni, tuzo ya mkimbiaji bora kwa upande wa wanaume ilimwendea Letsile Tebogo wa Botswana licha ya kunyakua tuzo ya mwanariadha bora wa mwaka huku upande wa wanawake tuzo hiyo ikishindwa na mkimbiaji Sydney McLaughin-Levrone wa USA.
Katika michezo ya uwanjani, Yaroslava Mahuchikh wa Ukraine alishinda kwa wanawakehuku tuzo hiyo ikimwendea Mondo Duplants wa Uswisi. Aidha michezo ya nje ya uwanja, tuzohizo ziliwaendea Tamirat Tola wa Ethiopia kwa wanaume huku kwa wanawake tuzo hiyo ilinyakuliwa na Sifan Hassan wa Uholanzi.
Hata hivyo, Wakenya waliokuwa wameteuliwa kuwania tuzo hizo hawakufanikiwa kuzishinda. Benson Kipruto na Agnes Ng’etich walikuwa wameteuliwa kuwania tuzo za wanariadha bora wa nje ya uwanjani huku Emmanuel Wanyony, Beatrice Chebet na Faith Kipyegon wakiteuliwa kuwania kwenye kitengo cha wakimbiaji bora.
Aidha tuzo ya wanariadha bora chipukizi kwa upande wa wanaume na wanawake iliwaendea Sembo Almayew wa Ethiopia na Mattia Furlani wa Italia mtawalia. Almayew ana umri wa miaka 19 sawia na Mattia Furlani.