logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Olunga Avunja Ndoa na Al Duhail, Aanza Mahusiano na Al Arabi

Uhamisho wa Olunga unafuatia kipindi cha mafanikio cha miaka minne katika klabu ya Al Duhail SC.

image
na Tony Mballa

Michezo06 July 2025 - 11:48

Muhtasari


  • Akiwa Japan, alishinda Kiatu cha Dhahabu cha Ligi ya J1 mwaka 2020 baada ya kufunga mabao 28 akiwa na Kashiwa Reysol na pia alitunukiwa tuzo ya Mchezaji Bora wa msimu (MVP).
  • Msimu wa mwaka 2019 katika Ligi ya J2 ulikuwa wa kusisimua pia, alikifungia klabu hiyo mabao 27.

Mshambuliaji wa Kenya, Michael Olunga, amejiunga rasmi na klabu ya Al Arabi SC ya Qatar kwa mkataba wa miaka miwili, hatua inayowakilisha sura mpya muhimu katika taaluma yake ya soka iliyopambwa na mafanikio.

Olunga anakuwa Mkenya wa pili kuchezea Al Arabi, akifuata nyayo za Dennis Oliech, ambaye aliwahi kuichezea klabu hiyo zaidi ya miongo miwili iliyopita.

Uhamisho wa Olunga unafuatia kipindi cha mafanikio cha miaka minne katika klabu ya Al Duhail SC, ambako aliaga akiwa mfungaji bora wa muda wote wa klabu hiyo, akifunga jumla ya mabao 130 katika michuano yote.

Michael Olunga

Uwezo wake wa kufumania nyavu ulimfanya atambe katika Ligi Kuu ya Qatar (Qatar Stars League), akiisaidia Al Duhail kutwaa mataji kadhaa huku akivutia heshima na pongezi kutoka pande zote.

Kabla ya mafanikio yake nchini Qatar, Olunga alikuwa amewika katika ligi mbalimbali duniani mbali na kipindi chake katika vilabu tofauti vya Ligi Kuu ya Kenya.

Akiwa Japan, alishinda Kiatu cha Dhahabu cha Ligi ya J1 mwaka 2020 baada ya kufunga mabao 28 akiwa na Kashiwa Reysol na pia alitunukiwa tuzo ya Mchezaji Bora wa msimu (MVP).

Michael Olunga

Msimu wa mwaka 2019 katika Ligi ya J2 ulikuwa wa kusisimua pia, alikifungia klabu hiyo mabao 27.

Katika soka ya kimataifa, aliwahi pia kucheza Uhispania akiwa na Girona, Sweden katika klabu ya Djurgården, na China na klabu ya Guizhou Heng Feng.

Kwa sasa, tetesi kuhusu mustakabali wake zimefikia kikomo, na Olunga anakumbatia changamoto mpya akiwa na Al Arabi, ambao wanatumai mshambuliaji huyo mrefu ataendeleza ubabe wake wa kufunga mabao na kuongoza juhudi za klabu hiyo katika mashindano ya ndani na ya kimataifa.

Michael Olunga

Akiwa na jumla ya mabao 273 katika zaidi ya mechi 320 za klabu alizochezea katika taaluma yake, Olunga bila shaka ni mmoja wa washambuliaji hatari zaidi kutoka Afrika.

Ustadi wake wa kufunga, uwezo wa kuzoea mazingira mapya, na wepesi wake mbele ya lango vimemfanya kuwa mmoja wa wachezaji wa kuaminika zaidi katika historia ya soka ya Kenya.

Ingawa Olunga anatarajiwa kukosa mashindano ya CHAN 2024, mashabiki bado wana matumaini kuwa nyota huyo ataendelea kuimarika na kuleta mchango muhimu katika kampeni ya Harambee Stars ya kufuzu Kombe la Dunia la 2026 katika mechi zijazo za kimataifa dhidi ya Gambia.

Michael Olunga

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved