Mtangazaji Lulu Hassan amedokeza wazi kwamba anafurahi kufanya kazi na mumewe na anatamani vituo vyote vya habari vingekumbatia mtindo huo.
Akizungumza katika mahojiano na kituo kimoja cha redio nchini, Lulu alisema kwamba amepata wakati mwepesi sana kufanya kazi mumewe kwa sababu tayari alikuwa rafiki yake.
“Unajua Rashid ni rafiki yangu, kwa hiyo inakuwa rahisi kufanya kazi. Natamani vyombo vyote vya habari vingekumbatia mtindo huu,” Lulu alisema.
Hata hivyo Lulu alisema kwamba kuna changamoto za kufanya kazi na mpenzi wake, kwa sababu kuna muda wanakuwa na mvurugano nyumbani ila inawalazimu kuonyesha nyuso za raha wanapokuwa hewani.
Aidha alimsifu Rashid akisema kwamba yeye hufanya kila awezalo kuhakikisha wanasuluhisha matatizo yao na kujenga mazingira mazuri ya kuishi pamoja na kufanya kazi.
Vilevile alisema iwapo televisheni zote zingekumbatia mtindo huo wa mke na mume kufanya kazi pamoja, sekta hiyo ingekuwa mbali sana.
Ikumbukwe kwamba hao ndio wanandoa wa kwanza kabisa kuwahi tangaza kwenye televisheni humu nchini, huku asilimia kubwa ya mashabiki ikitokea kukubali kazi yao.
