Muigizaji Wambui Nganga almaarufu Shipira amepuuzilia mbali madai ya kuwa kwenye ndoa na aliyekuwa muigizaji mwenzake katika kipindi cha The Real Househelps of Kawangware David Marucha (Michereti).
Mwaka wa 2019 uvumi uliibuka kuwa waigizaji hao wawili walikuwa wakipanga kufunga pingu za maisha. Walidaiwa kuwa wamechumbiana kwa muda mrefu na hata kubarikiwa na mtoto wa miaka mitano pamoja.
Wambui sasa ameweka wazi kuwa hizo zilikuwa fununu tu ambazo zilimshtua pia kama vile Wakenya wengine wengi.
"Nilishangaa, nilishtuka. Hadi kulikuwa na picha kuthibitisha kuwa niko na mtoto na Michereti. Ilikuwa ni picha ya kuigiza watu wakaanza tetesi," alieleza akiwa kwenye mahojiano na Jeff Kuria.
Muigizaji huyo alisema licha ya madai hayo kuwa ya uwongo yalikuwa ya baraka pia kwani yaliongeza wafuasi wake kwenye YouTube.
"Wafuasi waliongezeka kutoka 200 mpaka 7000 kwa siku moja," alisema.
Taaluma ya uigizaji wa Wambui kwenye YouTube ilianza vyema baada ya tetesi za mahusiano yake na Michireti.
Muigizaji huyo kutoka kaunti ya Nyandarua amefichua kuwa kwa sasa hayupo kwenye mahusiano yoyote.
"Sichumbiani. Sijui kama ni kukosa, ama huwa wanaangalia wanaona mimi ni wa mzaha," alisema.
Alitangaza kuwa anatafuta mchumba aliye na uwezo wa kifedha. Aidha alisema mwanaume anayeazimia kujitosa kwenye mahusiano naye ni sharti amkubali jinsi alivyo na awe tayari kumuunga mkono.
"Niko sokoni. Niko upande ambapo mtu hawezi kujitetea bei," alisema.
Wambui aliigiza kwenye Real Househelps of Kawangware kati ya mwaka wa 2018 na 2020. Katika kipindi hicho alishirikishi katika takriban vipindi 80 vya shoo hiyo iliyopeperushwa kwenye KTN na NTV.