
Gavana wa Kisumu, Profesa Anyang’ Nyong’o, amewapongeza wakazi wa kaunti hiyo kwa kudumisha amani wakati wa maandamano ya Jumatano.
Katika taarifa iliyotolewa na afisi ya gavana, Nyong’o aliwasifu wakazi kwa kujiheshimu na kuendesha shughuli zao kwa utulivu.
“Ningependa kuwashukuru wakazi wa kaunti ya Kisumu kwa kudumisha amani leo wakati wa shughuli za kuadhimisha mwaka mmoja wa maandamano ya Gen Z,” alisema.
Gavana aliongeza, “Wakazi wa Kisumu daima watakuwa makini kulinda na kukuza haki za binadamu katika jamhuri yetu.”
Pia alisisitiza kujitolea kwa kaunti katika kushiriki mijadala ya kiraia yenye kujenga.
“Tutaendelea kueleza kutoridhika kwetu kwa njia ya kujenga dhidi ya aina yoyote ya ukandamizaji wa kisiasa na ukiukaji wa haki za binadamu.”
Maandamano ya Gen Z, yaliyolipuka katikati ya mwaka 2024, yaliendeshwa na vijana wa Kenya waliotumia mitandao ya kijamii kuhamasisha maandamano ya kitaifa kupinga hatua mpya za ushuru na utawala mbaya.
Kisumu, ambayo mara nyingi huchukuliwa kuwa kitovu cha harakati za kisiasa, ilikuwa miongoni mwa maeneo yaliyoshuhudia mvutano mkubwa wakati wa wimbi la kwanza la maandamano hayo.
Hata hivyo, mwaka huu, jiji hilo lililoko kando ya Ziwa Victoria lilisalia na utulivu, huku wakazi wakiendelea na shughuli zao za kawaida japo maandamano ya kuadhimisha siku hiyo yalishuhudiwa katika kaunti nyingine.
Baadhi ya wanaharakati wa haki za binadamu waliokuwa wakizungumza na wanahabari walivurugwa na vijana waliokuwa wakitumia pikipiki, ambao baadaye waliondoka. Hakuna tukio kubwa lililoripotiwa mjini humo.