
Mwanaharakati wa haki za binadamu Boniface Mwangi anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumatatu, Julai 21, 2025.
Mwangi alikamatwa kwake katika operesheni ya polisi ambayo mamlaka zinadai ilizalisha ushahidi unaohusishwa na ugaidi.
Mkewe, mwanahabari na mwanaharakati Hellen Njeri Mwangi, alizungumza nje ya Kituo cha Polisi cha Pangani ambapo Mwangi anazuiliwa.

Njeri alithibitisha kuwa Mwangi alipelekwa makao makuu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) ili kutoa taarifa lakini alikataa kusaini baadhi ya nyaraka.
“Alikamatwa jana na walituruhusu kumuona. Asubuhi hii walimpeleka makao makuu ya DCI kuandika maelezo, lakini alikataa kusaini yale walikuwa wanataka. Kisha walimrudisha hapa Pangani. Kesho atafikishwa mahakamani, sijui ni kwa mashtaka gani,” alisema.
Njeri alidai kuwa kuna njama ya serikali kumbambikizia Mwangi mashtaka ya ugaidi, akisema maafisa wa polisi walitaja kutafuta vilipuzi wakati wa kumkamata.
“Watu hukusanya maguruneti ya machozi. Polisi walipokuja, ilikuwa kama tayari walijua wanachokitafuta, na hicho ndicho waliandika kwenye ripoti. Unaweza kuona nia yao ni kuhakikisha wanampata na kumshikisha kwa chochote… wanataka kusema hiyo ni hatua ya kigaidi,” alisema.
“Kwa kweli walisema wanatafuta vilipuzi. Kwa nini tuweke vilipuzi katika ofisi yetu wenyewe? Wana nia ya dhati kutumia chochote kumchomea Bonnie na kuhakikisha mashtaka yanadumu,” aliongeza.

Kulingana na taarifa ya DCI iliyochapishwa kwenye ukurasa wao wa X mnamo Julai 20, 2025, kukamatwa kwa Mwangi kulifuatia msako maalum nyumbani kwake, ambapo maafisa walipata simu mbili za mkononi, kompyuta mpakato na daftari kadhaa.
Baadaye alipelekwa katika ofisi yake ya Mageuzi Hub kwenye Barabara ya Rose, Hurlingham, ambapo msako wa pili ulifanyika.
“Wakati wa ukamataji, maafisa walipata simu mbili za mkononi, kompyuta mpakato na daftari kadhaa. Baadaye alipelekwa ofisini kwake Mageuzi Hub, Barabara ya Rose Hurlingham, ambapo msako mwingine ulifanyika na kukamatwa vifaa tisa vya kuhifadhi data (external hard drives), kompyuta mbili za ziada, mihuri ya kampuni za Brave Media Ltd na Courage Ltd, stempu ya kampuni, vitabu sita vya hundi, nakala za stakabadhi za kodi ya stempu, maguruneti mawili ya machozi ambayo hayajatumiwa, na risasi moja tupu ya milimita 7.62,” ilisoma taarifa ya DCI.
Mamlaka zimesema vifaa hivyo vitatumika kama ushahidi wakati wa kuwasilisha kesi mahakamani.

