
Bw. Samuel Njau Gicheru, mkazi wa Kirigiti katika Kaunti ya Kiambu, amemkaribisha Rais William Ruto katika eneo la Mlima Kenya kabla ya ziara yake iliyopangwa wiki ijayo.
Njau, ambaye anafanana sana na aliyekuwa Rais Mwai Kibaki, alitoa ujumbe wake kwenye video huku akimwiga Kibaki kwa sauti na mtindo wake, akieleza furaha ya wenyeji kuhusu ujio wa Rais.
Akizungumza kwenye video hiyo iliyosambazwa mtandaoni, Njau alisema wakazi wa Kirigiti wanamsubiri kwa hamu Rais Ruto, akimkumbusha kuwa eneo hilo ndilo lililoshuhudia mkutano wake wa mwisho wa kampeni kabla ya uchaguzi wa 2022.
Mbali na kumkaribisha Rais, Njau alitumia fursa hiyo kumwomba Ruto kujenga choo cha umma katika eneo la Kirigiti ili kusaidia wafanyabiashara wa soko.
"Habari, Rais Ruto. Habari yako? Tunaskia unakuja Mlima Kenya, na sote tuko na furaha na tunakusubiri kwa hamu. Niko hapa Kirigiti, mahali ulifanya kampeni yako ya mwisho, na tunakungoja kwa hamu," alisema Njau.
Aidha, alimuomba Rais aambatane na Naibu Rais Kithure Kindiki wakati wa ziara hiyo, akisema wakazi hawajamuona kwa muda mrefu.
"Hapa Kirigiti, hatuna mambo mengi. Sisi ile kitu tunataka ni choo cha umma, maana huwa tunaenda huko nyuma ya maduka na soko, na kuna kina mama. Hiyo inatosha," alisema.
"Lakini pia ni muhimu, wakati ule unakuja, utuletee Kindiki tumsalimie, maana hatujamuona. Na hiyo kitu ingine, ni lazima utuletee chapati, kila mtu tatu. Mambo ya soda mimi nitasimamia. Si namna hiyo?" aliongeza.
Ujumbe wa Njau unakuja wakati ambapo Rais William Ruto anapanga ziara yake katika maeneo mbalimbali ya Mlima Kenya kuanzia Aprili 1.
Rais Ruto anatarajiwa kuanza ziara yake ya siku tano katika eneo la Mlima Kenya, ikiwa ni mara yake ya kwanza kurejea katika eneo hilo baada ya miezi sita. Ziara yake inajiri wakati wa msisimko wa kisiasa, kufuatia kung’olewa kwa aliyekuwa naibu wake, Rigathi Gachagua.
Ratiba yake inajumuisha ziara katika kaunti saba, ambapo atakutana na wakazi, kukagua miradi ya maendeleo, na kushughulikia masuala muhimu ya eneo hilo.
Ratiba ya Ziara:
Jumanne, Aprili 1: Kaunti za Laikipia na Nyeri
Jumatano, Aprili 2: Kaunti za Meru na Kirinyaga
Alhamisi, Aprili 3: Kaunti za Nyandarua na Murang’a