
Atletico Madrid iliandamwa na bahati mbaya tena mbele ya Real Madrid katika mikwaju ya penalti, lakini safari hii kilicholeta mjadala ni penalti ya Julian Alvarez iliyokataliwa kwa utata, hali iliyogharimu timu ya Diego Simeone nafasi yao katika Ligi ya Mabingwa.
Katika pambano la hatua ya 16 bora lililopigwa Jumatano usiku, Atletico Madrid ilishinda mechi ya marudiano 1-0, shukrani kwa bao la mapema la Conor Gallagher baada ya sekunde 27 pekee.
Ushindi huo ulisawazisha matokeo ya jumla kuwa 2-2, lakini hakuna timu iliyoweza kupata bao la ushindi katika muda wa kawaida wala muda wa ziada, hivyo mechi ikaamuliwa kwa penalti.
Hii ilikuwa mara ya sita katika historia ya michuano ya mtoano kwa majirani hawa kupambana kupitia mikwaju ya penalti – na kwa mara nyingine tena, Real Madrid wakaibuka washindi kwa penalti 4-2.
Hata hivyo, penalti tata ya Julian Alvarez ndiyo inayoendelea kuzua gumzo.
Baada ya penalti tatu za mwanzo kufungwa kwa mafanikio, Alvarez alipata nafasi ya kuisawazishia Atletico kuwa 2-2. Akiwa kwenye mkwaju wake, mshambuliaji huyo wa Argentina aliteleza, lakini bado akafanikiwa kupasia nyavu. Mashabiki wa Atletico walishangilia wakiamini bao hilo limekubaliwa.
Hata hivyo,
sekunde chache baadaye, refa wa Poland, Szymon Marciniak, alifuta penalti hiyo
baada ya VAR kuingilia kati. Kulingana na picha za marudio, Alvarez aligusa
mpira mara mbili – mguu wake wa kushoto ukigusa kabla ya mguu wa kulia kupiga
mkwaju.
Katika uwanja wa Cívitas Metropolitano, ubao wa matokeo ulionyesha 2-2, jambo lililoongeza mkanganyiko. Lakini, kwa mujibu wa sheria, penalti hiyo haikuhesabiwa, na Real Madrid wakaendelea kuongoza 3-1.
Sheria ya 14.1 ya IFAB kuhusu penalti inasema: "Mchezaji anayepewa penalti haruhusiwi kuugusa mpira tena hadi pale utakapoguswa na mchezaji mwingine."
Hii ndiyo sababu hata mpira unapogonga mwamba kisha kurudi kwa mchezaji huyo, haruhusiwi kufunga kabla ya mwingine kuugusa.
Baada ya mechi, kocha wa Atletico, Diego Simeone, alieleza mashaka yake kuhusu uamuzi huo.
"Refa alisema Alvarez aligusa mpira kwa mguu wa kushoto kabla ya kuupiga, lakini mpira haukusogea," alisema. "Sijawahi kuona penalti inayopigwa kisha VAR iitwe kuikagua. Nataka kuamini waliona kitu, lakini je, kuna yeyote hapa aliyemwona akigusa mara mbili? Naona hakuna anayenyanyua mkono… basi, swali linalofuata tafadhali."
Kwa upande mwingine, kocha wa Real Madrid, Carlo Ancelotti, alisisitiza kuwa uamuzi ulikuwa sahihi:
"Waliliona kupitia VAR. Nilipata nafasi ya kuangalia na nadhani kweli aligusa mara mbili," alisema.
Kipa wa Real
Madrid, Thibaut Courtois, pia alikubaliana na uamuzi huo akisema:
"Nilihisi kuna kitu kisicho cha kawaida, nikamwambia refa. Alvarez
aliuteleza na kugusa mara mbili, kwa hiyo penalti haikuhesabiwa. Ni bahati
mbaya kwake, lakini ndivyo sheria inavyosema."
Atletico ilipata tumaini kidogo baada ya Jan Oblak kuokoa penalti ya Lucas Vazquez, lakini Marcos Llorente akagonga mwamba.
Hatimaye, penalti
ya Antonio Rudiger iliihakikishia Real Madrid ushindi wa 4-2, na kwa mara
nyingine, Atletico wakaondolewa kwa mikwaju ya penalti.
Kwa wafuasi wa Atletico, penalti ya Alvarez inabaki kuwa alama ya maswali. Kwa Real Madrid, ni ushahidi wa jinsi bahati inavyowaandama mahasimu wao wa jiji kila wanapokutana kwenye mikwaju ya penalti.