

KENNEDY amezungumzia kina cha uhusiano wake na mwanawe mkewe, Amber Ray – Gavin.
Akizungumza na Dr Ofweneke kupitia podkasti yake, Rapudo alisema kwamba kuishi na kijana huyo tineja ni jambo la kujivunia akimtaja kama mtoto ambaye amelelewa katika maadili ya kupendeza.
“Gavin ni mvulana ambaye ana maadili mazuri sana, mamake kwa kweli amemlea na kumkuza katika njia nzuri na hatujawahi kuwa na matatizo,” Rapudo alisema.
Baba huyo wa watoto 3 alifichua kwamba mara kwa mara huwa wanazungumza ya kiume na Gavin.
“Huwa tunakuwa na mazungumzo ya kiume. Wakati ninaona kitu Fulani hakiko sawa au wakati nina changamoto kidogo huwa namwaambia, ‘unajua nini mbona tusitoke na gari?’… na huwa tunatoka na kuzungumza.”
“Halafu pia huwa namwambia jinsi ya kushughulikia baadhi ya masuala kama kuburuzwa mitandaoni, shuleni na wanafunzi wenzake na ni bwana mdogo mzuri sana.”
Kuhusu mtoto huyo kumuita baba, Rapudo alifichua kwamba muda wote huo, hujawahi fanya uthubutu wa kumuita ‘baba’.
“Hapana, hujawahi niita babake. Kwa nini? Kwa sababu babake yuko hai. Na mara moja moja huwa wanakutana. Hivyo siwezi kumlazimisha kuniita baba wakati babake mwenyewe yuko hai. Ni kesi sawia, huwa binti yangu anaita babake Gavin ‘baba’? hapana! Kwa sababu mimi kama baba niko hai na tunaheshimu hii mipaka yote na kila kitu kinaenda sambamba,” Rapudo alijieleza kwa maelezo ya kuridhisha.
Rapudo na Amber Ray ni wanandoa wachache ambao wana ufanisi mkubwa katika kuendesha familia mseto – kila mmoja akiwa na mtoto kutoka kwa uhusiano wa awali.
Amber Ray kabla hajaolewa na Rapudo, alikuwa na mtoto wa kiume – Gavin – ambaye ni tineja.
Kwa upande mwingine, Rapudo kabla hajapata mtoto na Amber Ray miaka miwili iliyopita (Africana), alikuwa na watoto wawili kutoka kwa mahusiano yake ya awali.
Alimueleza Ofweneke kwamba alipata mtoto wake wa kwanza, binti wa miaka 13 wakati alikuwa chuo kikuu mwaka wake wa pili.
Baadae pia alikuja kupata mtoto wake wa pili – mvulana, ambaye alilazimika kuelekea mahakamani miezi kadhaa iliyopita ili kupata idhini ya kuonana naye mara kwa mara baada ya kile alichokitaja kuwa mamake alikuwa mwenye drama nyingi.