
BOSI wa lebo ya WCB Wasafi, Diamond Platnumz ameelekea mahakamani kumshtaki mpenzi wake wa zamani kwa kile alisema kwamba anatumia picha za zamani wakiwa pamoja kumchafulia jina.
Akithibitisha hatua hiyo kupitia ukurasa wake wa Instagram,
Diamond alisema kwamba mwanamke huyo ambaye hakuweka wazi utambulisho wake
amekuwa akimchafulia jina kwa kutumia video za zamani wakiwa pamoja.
Msanii huyo alithibitisha kwamba ameona baadhi ya video hizo
zikisambazwa na mpenzi wake wa zamani mitandaoni kwa lengo la kumharibia jina
licha ya kuachana muda mrefu uliopita.
“Nimeona kuna clip
zinasambazwa mtandaoni zinazonihusu…clip hizo ni za zamani, mwaka 2023, na zina
zaidi ya miaka miwili nyuma…na mwanamke huyo pia niliachana nae takriban miaka
miwili sasa,” Diamond alisema.
Msanii huyo alieleza
kwamba video hizo zinalenga kumharibia hata penzi lake la sasa na Zuchu,
akiweka wazi kwamba alishamjulisha mpenzi wa sasa kuhusu kumalizika kwa penzi
hilo la zamani.
“Lakini pia nilimueleza mwenzangu niliye nae na tukasameheana na kuanza
maisha mapya…” alisema.
Baada ya kugundua kwamba lengo la mwanamke huyo kutumia
video hizo za zamani wakiwa pamoja ni kumharibia, Diamond alisema tayari
amelikabidhi mikononi mwa idara husika kisheria.
“Mwanamke huyo sasa ameamua kutumia clip hizo na kuambatanisha na jumbe za uongo kwa lengo la kuni blackmail na kutengeneza fedha, jambo hili lishafikishwa katika mamlaka husika na taratibu za kisheria zinafuatwa. Shukran,” alisema.
Ungamo la Diamond kwamba alikuwa na mpenzi ambaye waliachana
miaka miwili iliyopita liliwaacha wengi na maswali mengi wasiweze kung’amua
utambulisha kamili wa mpenzi huyo.
Ifahamike mpenzi wa mwisho kuachana na Diamond kabla ya
Zuchu alikuwa ni Mkenya, Tanasha Donna ambaye waliachana mwishoni mwa mwaka
2020.
Miaka miwili baadae, 2022 – Diamond alidokeza kwa mara ya
kwanza kuwa katika mahusiano ya kimapenzi na Zuchu ambaye wamekuwa naye kwa
kipindi chote hadi sasa, japo katika uhusiano usioeleweka, baridi-joto.
Lakini je, mpenzi huyu wa 2023 ni nani?