
MALKIA wa muziki kutoka lebo ya WCB Wasafi, Zuchu ameibuka na kueleza bayana mahaba yake kwa bosi na mpenzi wake, Diamond Platnumz wiki kadhaa baada ya kuonekana mfarakano baina yao.
Wawili hao waliepeleka mahaba yao wazi wazi kwenye Instagram
ambapo Diamond alichapisha aya ndefu ya kusifia mapenzi na uwepo wa Zuchu
katika maisha yake.
Diamond alisema anakosa maneno ya kuelezea utamu na uzuri wa
Zuchu, akisema kwamba upendo kwake umepita viwango vya kuhesabika.
“Lile neno Mtamu Kama
“Nini”…. Ama Mzuri Kama “Nini”…..ama Nampenda Kama “Nini”… ile “Nini” ambayo
Upendo, Uzuri, Utamu na Thamani yake imepitiliza hadi Haielezeki basi ndio wewe
kwangu…” Diamond alijimaliza kwake Zuchu.
Vile vile, Diamond alifichua kwamba huenda kuna mipango ya
harusi na Zuchu, jambo ambalo alilielezea kama ‘siku kuu inayosubiriwa’.
Akisifia uzuri na utamu wa Zuchu, Diamond alisema kwamba ni
wengi aliowahi kuwa nao kimapenzi lakini pendo la Zuchu kwake limezidi wengine
wote na kumtaja kama funga-kazi.
“Wengi niliwahi kuwa nao lakini hapajatokea aliewahi kupendwa nami
zaidi yako and I can not wait for our big day…Unaniangusha tu kwa kuto kujua
huyu fala Anakupenda kias gani na kuacha hawa Nzi wa Mitandaoni wakuendeshe kwa
kutumia tuvituvitu vya kwenye kazi yangu…hawa hautakiwi kuwajibu kwa Reaction
yoyote zaidi ya Kuenjoy Maisha na kufurahia Baraka tulizojaaliwa na Mwenyez
Mungu - Happy Valentine Zuuh , Happy Valentine Nini,” Diamond alizidi
kujilipua.
Kwa upande wake, Zuchu aliyeitwa king’ang’anizi na mfanyikazi
wa Wasafi FM, Juma Lokole, aliweka wazi hisia zake kwa Diamond akisema kwamba
kwake hatoki hata waseme nini.
“I love you More Pole kwa
kuchelewa kujibu nakupenda.️ Ninashukuru kwa ajili yako na siendi popote,” Zuchu alidamka.
Wiki chache zilizopita, Juma Lokole wakati anamhoji kakake
Diamond kuhusu uwezekano wa msanii huyo kumuoa Zuchu, alisema kwamba baadhi
wanahisi Zuchu anang’ang’ania penzi la Diamond ambaye anaonekana kutokuwa na
haja naye.
Tamko hili lilimkirihi Zuchu ambaye alikwenda kwenye
Instagram na kuachia onyo kali akitishia kuelekea mahakamani ikiwa hawatoachana
kumjadili kwenye vipindi vyao.