logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Itabidi mpunguze propaganda la sivyo tutauliza serikali idhibiti social media – Atwoli

“Ni lazima mpende nchi hii, msipopenda nchi hii waajiri watahama, ama kama si hivyo mtaanza kulimana, mkianza kupigana tunakuwa kama wenzetu Sudani, Kongo, Somalia na wengine.”

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari06 April 2025 - 10:45

Muhtasari


  • “Kenya ni setellite ya shughuli za kiuchumi katika kanda hii, hata tukipiga kelele, wale wenzetu Tanzania, Uganda wanataka Kenya sana kwa sababu ya mifumo ya mawasiliano tuliyo nayo.”
  • Alisema kwamba mataifa Tajiri kama vile China na mengine yamedhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii na hiyo ndio salama ikiwa matumizi yake yatakuwa yanatishia usalama wa nchi.

Francis Atwoli, katibu wa COTU

KATIBU mkuu wa muungano wa wafanyikazi humu nchini COTU, Francis Atwoli ametaka watumizi wa mitandao ya kijamii kupunguza kasi ya kile alichokitaja kama kueneza propaganda na siasa za chuki kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii humu nchini.


Akizungumza katika mkutano wa wajumbe wa COTU Jumamosi, Atwoli alisema kwamba nchi nyingi tu za Afrika zinatamani utulivu na amani iliyoko Kenya, akionya kwamba watumizi wa mitandao ya kijamii wanataka kuharibu sifa hiyo zuri ya taifa.


“Kenya ni setellite ya shughuli za kiuchumi katika kanda hii, hata tukipiga kelele, wale wenzetu Tanzania, Uganda wanataka Kenya sana kwa sababu ya mifumo ya mawasiliano tuliyo nayo.”


“Sasa viwanda haviwezi kuhama na hapa ndio kuna kila kitu, isipokuwa kitu naomba tu wale watu wetu wa mitandao ya kijamii, itabidi mpunguze propaganda. Ni lazima mpende nchi hii, msipopenda nchi hii waajiri watahama, ama kama si hivyo mtaanza kulimana, mkianza kupigana tunakuwa kama wenzetu Sudani, Kongo, Somalia na wengine,” Atwoli alisema.


Kiongozi huyo alisema kuwa ikiwa watumizi wa mitandao ya kijamii wasipopunguza kasi ya kueneza propaganda itabidi wao kama muungano wa wafanyikazi wameiandikia serikali barua ya kutaka kudhibitiwa kwa shughuli za mitandaoni kwa Wakenya.


Alisema kwamba mataifa Tajiri kama vile China na mengine yamedhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii na hiyo ndio salama ikiwa matumizi yake yatakuwa yanatishia usalama wa nchi.


“Hatutaki kuenda njia kama ya hayo mataifa yenye mizozo, lakini watu wa mitandao ya kijamii wanatuelekeza huko. Unajua sasa itabidi, na hatukutaka hivyo, itabidi tuulize serikali idhibiti mitandao ya kijamii,” alitishia.


“Kama China wamedhibiti, TikTok ya China ni yao, sio hii yenu hapa, mambo ya WhatsApp hakuna China, Dubai, Cuba na hizi nchi zingine. Na ni lazima tuulize kwa sababu ukifungua TikTok siku hizi na Watoto wadogo wanajua kufungua, mambo mengine yanafanyika huko sijui kama ni mimi naona pekee,” aliongeza.


Alisisitiza akisema kuwa ikiwa mienendo hiyo chafu itaendelea basi Suluhu litakuwa kudhibitiwa kwa matumizi ya Wakenya kwenye mitandao ya kijamii.


 


 


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved