logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Ruto: AIPCA ni kanisa pekee la serikali, mafuta yenu ya Holy Oil yalinifanya kuwa rais

Alikumbuka kwamba kabla ya uchaguzi wa 2022, alihudhuria hafla ya Holy Oil ya kanisa la AIPCA kaunti ya Nyeri na wiki chache baadae akatwaa urais.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari18 April 2025 - 15:12

Muhtasari


  • Akizungumza Alhamisi katika kanisa la AIPCA jimbo la Meru katika sherehe ya mafuta matakatifu, Ruto alisema kwamba yeye ni mmoja wa wanufaikaji wakubwa kutokana na mafuta hayo.
  • Alikumbuka kwamba kabla ya uchaguzi wa 2022, alihudhuria hafla ya Holy Oil ya kanisa la AIPCA kaunti ya Nyeri na wiki chache baadae akatwaa urais.

Rais William Ruto katika kanisa la AIPCA, Meru//PCS

RAIS William Ruto amemiminia sifa dhehebu la AIPCA akidai kwamba ndilo kanisa pekee ambalo limesimama na kupigania serikali kwa muda mrefu.

Akizungumza Alhamisi katika kanisa la AIPCA jimbo la Meru katika sherehe ya mafuta matakatifu, Ruto alisema kwamba yeye ni mmoja wa wanufaikaji wakubwa kutokana na mafuta hayo.

Alikumbuka kwamba kabla ya uchaguzi wa 2022, alihudhuria hafla ya Holy Oil ya kanisa la AIPCA kaunti ya Nyeri na wiki chache baadae akatwaa urais.

“Hili ndilo kanisa la serikali. Mimi ningependa kutoa shukrani kwenu, hii Holy Oil, kabla hatujaenda uchaguzi 2022, nyinyi mnajua tulikuwa pale Nyeri, na nilikuja pale. Na kwa sababu ya maombi yenu na haya mafuta ya Holy Oil, si mimi ni rais wa Jamhuri ya Kenya leo? Si Bwana Yesu asifiwe jamani?”

“Mimi ni mnufaikaji na ningependa kuwaambia kwamba kwa sababu hii na maombi yenu, na mwenyekiti wetu mama hapa amesema mnaombea taifa letu la Kenya na mnaiombea pia. Wakati mwingine hamjui kama hayo maombi yanafika ama hayafiki. Wacha niwape hakikisho kwamba maombi mnaoniombea yanafika,” Ruto alisema.

Kiongozi wa taifa aliradidi kwamba anaendelea kupata nguvu ya kuchapa kazi kutokana na maombi ya Wakristo na haswa wale wa dhehebu la AIPCA.

“Nataka tu niwahakikishie kwamba hiyo kazi mliyonipatia kwa maombi yenu nak wa kura zenu, mimi nitafanya kwa bidii na kwa kujitolea. Na itafanyika, na tutamuaibisha shetani, mimi ndio nawaambia,” alisema.

Ruto alimaliza kwa kuomba msaada wa kanisa la AIPCA ambalo alidai yeye ni mshirika wake wa muda mrefu, kumsaidia kuunganisha Wakenya wote.

“Askofu, wewe ndiye kiongozi wetu wa kanisa hili na mimi ni member wa hili kanisa, nimesema mnisaidie tuunganishe taifa letu la Kenya. Na chochote kitakachohitajika, mimi kama kiongozi wa taifa hili nitafanya ili kuunganisha wananchi wote wa taifa hili,” Ruto alisema.

Katika ibada hiyo pia, kiongozi wa taifa alizidi kutetea serikali jumuishi akisema kwamba ni pana kiasi kwamba inaweza kujumuisha kila mmoja Kenya yote na si lazima mmoja aondoke ili kutengenezea mwingine nafasi.

 

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved