logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Guinea Yashirikiana na China Kufanikisha Nishati Endelevu

Awali, usiku wa Conakry ulitawaliwa na kelele za jenereta za dizeli, licha ya eneo hili kujulikana kama “Mnara wa Maji” wa Afrika Magharibi.

image
na XINHUA

Habari27 August 2025 - 18:55

Muhtasari


  • Mradi huu umewezesha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika mji mkuu wa taifa, Conakry, na vijiji vya milimani kaskazini.
  • Sasa kituo hiki kinaonekana kwenye noti ya franc 20,000 ya Guinea, hali iliyo tofauti kabisa na miaka kumi iliyopita.

CONAKRY, GUINEA, Agosti 27, 2025 — Katika Mto Konkoure unaotiririka kutoka nyanda za juu za Fouta Djallon katikati ya Guinea, jengo kubwa la Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta linaakisiwa kwenye maji.

Mradi huu umewezesha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika mji mkuu wa taifa, Conakry, na vijiji vya milimani kaskazini. Sasa kituo hiki kinaonekana kwenye noti ya franc 20,000 ya Guinea, hali iliyo tofauti kabisa na miaka kumi iliyopita.

Awali, usiku wa Conakry ulitawaliwa na kelele za jenereta za dizeli, licha ya eneo hili kujulikana kama “Mnara wa Maji” wa Afrika Magharibi. Zaidi ya asilimia 70 ya nishati ya Guinea ilitokana na mafuta mazito yenye gharama kubwa na uchafuzi mkubwa, hali ambayo ilikwamisha sana maendeleo ya kiuchumi.

Picha iliyopigwa Mei 3, 2025, inaonyesha noti ya franki 20,000 za Guinea yenye picha ya Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta, huku kituo hicho kikiwa nyuma yake huko Dubreka, Guinea. (CWE/Handout kupitia Xinhua)

“Kabla ya kujengwa kwa Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta, umeme ulikuwa unakatika mara kwa mara katika jamii yetu. Tulipata kukatika karibu kila siku, wakati mwingine kwa saa kadhaa,” anakumbuka Alhassane Bangoura, mkalimani wa eneo hilo aliyefanya kazi kwenye mradi huo.

Mnamo Agosti 2015, kituo hiki kilichopewa ujenzi na Kampuni ya China International Water and Electric Corporation (CWE), ambayo ni kampuni tanzu ya China Communications Construction Company Limited, kilianza kufanya kazi kikamilifu.

Picha ya angani iliyopigwa Aprili 25, 2025, inaonyesha mandhari ya Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta kilichoko Dubreka, Guinea. (Xinhua/Han Xu)

Kwa wastani, kituo hiki huzalisha zaidi ya kilowati-saa bilioni 1.125 za umeme safi kila mwaka, kikiwa kimepunguza kwa karibu nusu pengo la nishati nchini na kuongeza kiwango cha vyanzo mbadala vya nishati katika mchanganyiko wa nishati wa Guinea.

“Mtandao wa usafirishaji wa umeme uliojengwa sambamba na kituo hiki unasambaza nguvu kutoka mji mkuu hadi mikoa 11. Maeneo ya mbali yalipata umeme wa uhakika kwa mara ya kwanza,” alisema Djenabou Diallo, meneja wa fedha wa Kampuni ya Usimamizi ya Kituo cha Kaleta.

Mwaka 2021, Kituo kingine cha Umeme wa Maji cha Souapiti, pia kilichojengwa na CWE kando ya Mto Konkoure, kilianza kufanya kazi. Kwa pamoja, vituo vya Kaleta na Souapiti vyenye uwezo wa megawati 690 sasa huzalisha zaidi ya asilimia 80 ya nishati ya Guinea, na hivyo kuikomboa nchi kutokana na utegemezi wa mafuta mazito.

Nishati hii ya uhakika na rafiki kwa mazingira pia imegeuza Guinea kutoka taifa lililokuwa na upungufu wa nguvu hadi muuzaji wa umeme, ikiwasambazia majirani sita akiwemo Senegal, Gambia, Guinea-Bissau na Sierra Leone.

“Tulikuwa tukihangaika kukidhi mahitaji ya ndani. Sasa tunawasha taa katika nchi jirani,” Diallo aliambia Xinhua kwa fahari.

Picha iliyopigwa Aprili 24, 2025, inaonyesha jenereta za Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta kilichoko Dubreka, Guinea. (Xinhua/Han Xu)

Ndani ya chumba cha udhibiti cha Kaleta, Bangoura aliisaidia kwa ustadi timu ya wenyeji. Kama mwanakikosi wa uendeshaji wa kituo, safari yake inaonyesha pia uimara wa ushirikiano wa kiufundi kati ya China na Guinea.

“Tulipokea mafunzo ya kitaalamu kuanzia hatua ya ujenzi hadi uendeshaji—katika uhandisi wa umeme, kulehemu na matengenezo ya vifaa. Uhamishaji wa maarifa kutoka kwa wahandisi wa Kichina umetupa ujuzi wa thamani,” alisema.

Wakati wa kilele cha ujenzi, mradi wa Kaleta uliunda zaidi ya ajira 1,500 kwa wenyeji. Tangu hatua ya uendeshaji mwaka 2016, CWE imeshirikiana na serikali ya Guinea kuchagua karibu wanafunzi 100 wa Kiguinea kusomea China au vyuo vikuu vya ndani.

“Ukimpa mtu samaki unamlisha kwa siku moja, lakini ukimfundisha kuvua unamlisha maisha yote,” alisema Chen Qiuhan, mkurugenzi wa maendeleo ya soko wa CWE Guinea.

Wataalamu wa Kichina na Kiguinea wakifanya kazi pamoja katika chumba cha udhibiti cha Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta huko Dubreka, Guinea, Aprili 24, 2025. (Xinhua/Han Xu)

Mfumo wa mafunzo uliotekelezwa Kaleta ulirudiwa kwa mafanikio katika Souapiti. Wahandisi wengi wa Kiguinea waliopata mafunzo Kaleta sasa ndio wakufunzi wa mradi mpya. Leo, timu za wenyeji zinaweza kushughulikia matengenezo ya kila siku na kushiriki katika upangaji wa ratiba na uendeshaji wa vituo vyote viwili.

“Tulifunzwa sio tu teknolojia, bali pia falsafa ya maendeleo endelevu,” Bangoura alibainisha.

Timu ya mradi wa Kaleta pia ilitoa vifaa vilivyonufaisha zaidi ya wakaazi 20,000 wa karibu, huku “siku za wazi” mara kwa mara zikivutia mamia ya watoto wa eneo hilo.

“Wajenzi wa Kichina walicheza mpira nasi, walisherehekea sherehe zetu na kuheshimu utamaduni wetu kama marafiki. Wakati mmoja, ndugu yangu alipougua, mfanyakazi wa Kichina alisaidia kuwasiliana na timu ya madaktari wa Kichina na kutupeleka hospitalini,” Bangoura alisimulia.

Wataalamu wa Kichina na Kiguinea wakikagua vifaa katika Kituo cha Umeme wa Maji cha Kaleta huko Dubreka, Guinea, Aprili 24, 2025. (Xinhua/Han Xu)

Kadri giza linavyotanda, mwanga wa Kaleta huangaza kama nyota kwenye bonde. Majumbani, watoto husoma chini ya taa, viwanda hufanya kazi na mashine, na miji ya nchi jirani hunufaika na umeme wa Guinea.

“CWE imejitolea kuendeleza ushirikiano na serikali ya Guinea. Kwa kuimarisha sekta ya nishati, tunalenga kuunga mkono ndoto ya Guinea katika maendeleo ya sekta ya madini,” alisema Chen.

Noti ya franc 20,000 ya Guinea yenye picha ya kituo hiki sio tu ishara ya maendeleo ya taifa hili la Afrika Magharibi, bali pia ujumbe unaovuka milima na bahari: Ushirikiano wa kweli huhakikisha mwanga wa maendeleo unafika kila pembe.

 

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved