

Katika Rwanda ya Kusini, shule ya kiufundi inalima uyoga kwa kutumia teknolojia ya Juncao ili kuimarisha mpango wake wa chakula kwa wanafunzi — hatua bunifu ya kushughulikia changamoto za muda mrefu za lishe kwa njia ya gharama nafuu na endelevu.
Mpango wa chakula shuleni umekuwa sehemu muhimu ya sera ya elimu ya Rwanda, ukiwalenga kupunguza njaa miongoni mwa watoto wakati wa masomo na kupanua upatikanaji wa elimu, hasa kwa watoto kutoka familia zenye kipato cha chini.
Katika Shule ya Kiufundi ya Busasamana, mwalimu wa fizikia na mratibu wa mpango wa chakula shuleni, Alice Allouette Marie Munyurabanga, anaona kilimo cha uyoga kama njia yenye matumaini ya kuboresha ubora wa milo kwa wanafunzi.
“Kilimo cha uyoga kinatoa fursa mpya ya kuboresha milo tunayotoa, hasa kwa wanafunzi kutoka familia zinazokumbwa na changamoto za kifedha,” alisema.
“Mpango wa chakula mashuleni unakumbwa na changamoto halisi wakati wazazi wengine wanaposhindwa kuchangia kwa wakati,” alisema.
“Kilimo cha uyoga kinaweza kuwa chaguo zuri kujaza pengo hilo. Lakini hatuna maarifa na ujuzi wa kutosha kuhusu mbinu zinazohitajika kulima uyoga.”

Mtaalamu wa Juncao kutoka China, Hu Yingping, akitoa mhadhara kwa wanafunzi wa mafunzo katika Kituo cha Maonyesho ya Teknolojia ya Kilimo cha China-Rwanda kilichoko Wilaya ya Huye, Rwanda, tarehe 16 Julai 2025. (Huang Wanqing/Xinhua)
Aliyasema hayo katika mahojiano na shirika la habari la Xinhua wakati wa mafunzo ya teknolojia ya Juncao yaliyofanyika hivi karibuni katika Kituo cha Maonesho ya Teknolojia ya Kilimo kati ya China na Rwanda (C-RATDC) kilichoko Wilaya ya Huye, Mkoa wa Kusini mwa Rwanda.
Munyurabanga alikuwa miongoni mwa washiriki 57 kutoka nchi tano za Afrika waliokuwa wakihudhuria Warsha ya Pili ya Mafunzo ya Afrika kuhusu Matumizi ya Teknolojia ya Juncao, iliyofanyika kuanzia Julai 16 hadi Julai 23.
Warsha hiyo, iliyoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Idara ya Mambo ya Kiuchumi na Kijamii ya Umoja wa Mataifa, Wizara ya Kilimo na Mifugo ya Rwanda, na Chuo Kikuu cha Kilimo na Misitu cha Fujian nchini China, ililenga matumizi ya teknolojia ya Juncao katika kilimo cha uyoga, lishe ya mifugo, na utunzaji wa mazingira.
Iliwakutanisha maafisa wa kilimo, waalimu, na wataalamu wa maendeleo kutoka barani Afrika.
Mapema mwezi Mei, Munyurabanga alijiunga na ziara ya mafunzo nchini China, ambako alijifunza kwa mara ya kwanza kuhusu teknolojia ya Juncao. Alisema uzoefu huo uliamsha ari mpya ya kutaka kutumia ubunifu huo shuleni kwake.
“Kwa bahati, nilichaguliwa kushiriki katika mafunzo haya ya hivi karibuni ya kuongeza uwezo,” alisema.
“Nayaona kama fursa kubwa kwa shule yangu, na pia kwa nchi, kuongeza uelewa na kuboresha ujuzi wetu katika kilimo cha uyoga. Kwa maarifa niliyopata, nitaweza kusaidia kuzalisha uyoga wa kutosha kwa wanafunzi wetu nitakaporejea shuleni.”
Juncao ni aina ya majani mseto yaliyobuniwa miaka ya 1980 na Profesa Lin Zhanxi wa Chuo Kikuu cha Kilimo na Misitu cha Fujian. Ni teknolojia ya kilimo yenye matumizi mengi.

Kwa kiasi kikubwa, hutumika kama msingi wa kukuza uyoga wa chakula na wa dawa, lakini pia hutumika kama lishe ya mifugo na kusaidia katika urejeshaji wa ikolojia. Ubunifu huu umeanzishwa katika zaidi ya nchi 100, ikiwemo Rwanda.
Mradi wa teknolojia ya Juncao ulizinduliwa katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa mwaka 2017 na unaungwa mkono na Mfuko wa Amani na Maendeleo wa Umoja wa Mataifa.
Munyurabanga alisema uyoga ulipendekezwa kati ya mboga mbalimbali kwa sababu una virutubisho vya kutosha na ni wa gharama nafuu. Kwa sasa, shule yake hujumuisha uyoga kwenye milo ya wanafunzi angalau mara mbili kwa wiki.
Shule yake pia ina ardhi kubwa kwa ajili ya shughuli za kilimo.
Baada ya kurejea kutoka China, alianzisha teknolojia ya Juncao kwa wenzake kazini, ambao waliipokea kwa mikono miwili.

Tangu wakati huo, shule hiyo imeamua kupanda majani ya Juncao ili kuanza kuzalisha msingi wa kukuza uyoga wao wenyewe.
“Matumaini yangu ni kwamba shule yetu itakuwa mfano bora wa kilimo cha uyoga na uzalishaji wa msingi wa ukuaji wa uyoga,” alisema.
“Shule nyingine zitaweza kujifunza kutoka kwetu, siyo tu kuhusu jinsi ya kukuza uyoga, bali pia jinsi ya kuandaa msingi wake, kupika uyoga, na kuujumuisha kwenye milo ya wanafunzi.”
Baada ya kupata maarifa kuhusu mpango wa chakula mashuleni nchini Rwanda, Chen Xiaobin, mtaalamu kutoka C-RATDC, alisema anatarajia kuandaa warsha zaidi za mafunzo mahsusi kwa shule, kwa lengo la kuimarisha mkakati wa kitaifa wa chakula kupitia matumizi ya teknolojia ya Juncao.