logo

NOW ON AIR

Listen in Live

"Gen-Z walianguka na mimi!" Nakhumicha azungumzia maisha baada ya kupoteza kazi ya uwaziri

Alisema hakupata taarifa yoyote ya awali kuhusu kutimuliwa kwake, bali alipata habari hizo moja kwa moja kupitia matangazo ya TV.

image
na Samuel Mainajournalist

Yanayojiri08 March 2025 - 08:43

Muhtasari


  •  "Nilikuwa waziri wa afya, kisha mitandao ikaja, wakasema Gen Z wanaanguka na watu, wakaanguka na mimi," Nakhumicha alisema.
  •  Baada ya kuondolewa serikalini, Nakhumicha anasema sasa anajihusisha na kilimo, akizingatia upandaji na uuzaji wa kabeji.

Former Health CS Susan Nakhumicha / FILE

Aliyekuwa Waziri wa Afya, Susan Nakhumicha, amezungumzia maisha yake baada ya kutimuliwa kwenye baraza la mawaziri na Rais William Ruto mnamo Juni 2024.

 Nakhumicha alikuwa miongoni mwa mawaziri waliopigwa kalamu wakati Ruto alipovunja baraza lake lote, isipokuwa Waziri Mkuu Musalia Mudavadi, katika kile alichokiita juhudi za kuunda serikali yenye mshikamano wa kitaifa.

 Hatua hiyo ilijiri wakati wa maandamano makubwa yaliyoongozwa na vijana wa Gen Z, ambao walikuwa wakishinikiza mageuzi makubwa serikalini baada ya kupitishwa kwa Muswada wa Fedha wa 2024, ambao baadaye ulifutiliwa mbali. Maandamano hayo, yaliyoshuhudiwa kote nchini, yaliweka shinikizo kubwa kwa serikali, huku waandamanaji wakidai uwajibikaji zaidi kutoka kwa uongozi wa taifa.

 Akizungumza Ijumaa, Machi 7, mjini Kitale wakati wa ibada ya kumbukumbu ya aliyekuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Wafula Chebukati, Nakhumicha alieleza jinsi alivyopata habari za kufutwa kwake.

 "Nilikuwa waziri wa afya, kisha mitandao ikaja, wakasema Gen Z wanaanguka na watu, wakaanguka na mimi," Nakhumicha alisema kwa utani. 

Alifichua kuwa hakupata taarifa yoyote ya awali kuhusu kutimuliwa kwake, bali alijifunza habari hizo moja kwa moja kupitia matangazo ya moja kwa moja kwenye televisheni.

"Bishop amehubiri hapa akisema kuwa wakati wa Rais Moi matangazo yalikuwa kwa redio, lakini yetu haikuwa redio, ilikuwa kwa TV. Nilipoangalia, nikasikia baraza la mawaziri lote limefutwa kazi, nikaona watu wamefurahi kila mahali," aliongeza huku akitabasamu.

Nakhumicha, aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Afya mnamo 2022, alikuwa mmoja wa maafisa wa serikali waliokumbwa na hasira za umma, huku baadhi ya viongozi wa upinzani na wanaharakati wakimtuhumu kwa kushindwa kusimamia sekta ya afya ipasavyo.

Uamuzi wa Rais Ruto wa kuivunja serikali yake ulitokana na malalamiko makubwa ya wananchi kuhusu utendakazi wa mawaziri wake. Maandamano ya Gen Z yaliweka shinikizo kubwa kwa serikali, yakihimiza uwajibikaji na uwazi serikalini.

Katika hotuba yake ya Juni 2024, Rais Ruto alisema kuwa kuvunjwa kwa baraza la mawaziri kulilenga kuongeza uwajibikaji, ufanisi na uwazi katika utoaji wa huduma kwa wananchi. Alisema pia kuwa serikali mpya ingekuwa na sura ya taifa kwa kujumuisha viongozi kutoka mirengo mbalimbali ya kisiasa, ikiwa ni hatua ya kuleta mshikamano wa kitaifa.

 Baada ya kuvunjwa kwa baraza hilo, Ruto aliteua mawaziri wapya, huku baadhi ya sura mpya zikitoka ndani ya chama cha ODM cha Raila Odinga, ishara ya jaribio la kuunda serikali ya mseto. Hatua hii ilizua mjadala mkali kisiasa, huku baadhi ya wafuasi wa Kenya Kwanza wakilalamika kuwa Ruto alikuwa anawapa upinzani nafasi nyingi serikalini.

 Baada ya kuondolewa serikalini, Nakhumicha anasema sasa anajihusisha na kilimo, akizingatia upandaji na uuzaji wa kabeji katika eneo la Cheranganyi.

"Tangu siku hiyo, nimemtazamia Mungu. Sasa mimi nafanya ukulima, sina kazi, napanda na kuuza kabeji huko Cheranganyi," aliongeza. 

Licha ya kupoteza nafasi yake serikalini, Nakhumicha anasema anaendelea na maisha yake kama mkulima, huku akitazama mustakabali wake kisiasa.

Haijabainika ikiwa ana mipango ya kurejea kwenye ulingo wa siasa, lakini kwa sasa, anasema anajikita zaidi katika shughuli zake za kilimo.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved