logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Takriban watu 21 wafariki baada ya basi kuanguka kutoka kwenye daraja

Takriban watu 18 wamejeruhiwa, watano kati yao vibaya sana.

image
na Radio Jambo

Habari04 October 2023 - 03:57

Muhtasari


•Miongoni mwa waliofariki ni raia watano wa Ukraine, Mjerumani mmoja na dereva wa Italia, gavana wa jiji Michele Di Bari alisema.

•Takriban watu 18 wamejeruhiwa, watano kati yao vibaya sana.

Takriban watu 21 wakiwemo watoto wawili wamefariki baada ya basi kuanguka kwenye barabara ya juu karibu na mji wa Venice nchini Italia na kuwaka moto, maafisa wamesema.

Basi hilo lilivunja kizuizi na kutumbukia karibu na njia za reli katika wilaya ya Mestre, ambayo imeunganishwa na Venice kwa daraja.

Miongoni mwa waliofariki ni raia watano wa Ukraine, Mjerumani mmoja na dereva wa Italia, gavana wa jiji Michele Di Bari alisema.

Meya wa Venice Luigi Brugnaro alisema "janga kubwa" limetokea.

"Hakuna maneno yanayoweza kueleza tukio hilo," alisema kwenye mtandao wa kijamii.

Basi hilo linafikiriwa kukodishwa kuchukua watalii kati ya Venice na eneo la kambi katika wilaya ya karibu ya Marghera.

Kisa hicho kilitokea mwendo wa saa 19:45 (17:45 GMT) huku basi hilo likiripotiwa kuwarudisha watalii kwenye kambi hiyo.

Baadhi ya ripoti zinasema basi hilo lilikuwa linatumia gesi ya methane na kuangukia kwenye njia za umeme na kuwaka moto.

Waziri wa Mambo ya Ndani Matteo Piantedosi alionya kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeka.

Chanzo cha ajali hiyo bado hakijafahamika na waokoaji wanaendelea na kazi nayo katika eneo la tukio.

Takriban watu 18 wamejeruhiwa, watano kati yao vibaya sana.

Kituo cha mapokezi chenye watalaam wa kisaikolojia na magonjwa ya akili kimeanzishwa katika hospitali iliyo karibu ili kutoa msaada kwa familia za waathiriwa.

Waziri Mkuu wa Italia Giorgia Meloni alisema anafuatilia matukio na akatoa rambirambi zake.

"Mawazo yetu ni kwa waathiriwa na familia zao na marafiki," alisema.

Rais wa Tume ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen alisema anasimama na viongozi wa Italia "wakati huu wa maumivu makali".

Mnamo mwaka wa 2013, watu 38 waliuawa baada ya dereva kushindwa kudhibiti njia karibu na mji wa Monteforte Irpino kusini mwa Italia, na kugonga magari mengine kadhaa kabla ya kuanguka kwenye korongo.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved